Uhamasishaji wa Wananchi kushiriki Katika uchangiaji wa ujenzi wa kituo cha Afya Halmashauri ya Pangani umeanza
Halmashauri ya wilaya ya Pangani kupitia idara ya afya imeanza uhamasishaji wa ukarabati na ujenzi wa kituo cha afya cha Mwera kwa kuvishirikisha vijiji vya jirani ikiwa ni pamoja na kijiji cha Langoni wilayani humo.
Akizungumza na wananchi wa vijiji vya Mwera na Langoni kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Pangani Bwana Daudi Mlahagwa ameeleza kuwa ujenzi huo utazingatia mfumo wa force account hivyo wananchi wa vijiji hivyo wanatakiwa washiriki kwa kujitolea nguvu kazi.
‘’Nini ambacho watu wanatarajia na serikali inatarajia ni kuona kwamba hii fedha inatumika kwa utaratibu ambao umeelekezwa na serikali kwa hiyo mtaona kwamba muda tuliopewa sisi ni mfupi unaitaji sana ushirikiano, kwa hiyo tuombe tu kwamba ushiriki wa wananchi ni kitu cha msingi na ni lazima tufanye kwa muda ambao umeelekezwa’’ amesema Bwana Mlahagwa.
Nao wananchi wa vijiji hivyo hususani wakina mama wamesema kuwa wameupokea mradi huo na kuahidi kushiriki kwa dhati kwenye zoezi hilo la kujitolea nguvu kazi ili kuepuka adha ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma ya afya.
‘’Sisi wananchi wa kijiji cha Langoni tumeupokea vizuri kwa sababu mimi mwanangu alishawahi kuzaa eneo la Bweni kutokana na changamoto ya feri lakini kwa sasa tunaafurahia kweli tunaomba tu mradi uanze hata sasa hivi na tutatoa ushirikiano kwa nguvu zote.’’ Amesema mmoja wa wananchi.


Comments
Post a Comment